
NSAJIGWAKocha msaidizi wa timu ya Yanga, Shadrak Nsajigwa amekiri kuwa walipigana kufa au kupona kufika hatua ya makundi ya kombe la Shirikisho kwakua mchezo wa marudiano dhidi ya Welaita Dicha ulikuwa mgumu sana.
Nsajigwa ameyasema hayo katika uwanja wa ndege wa Mwalimu Nyerere baada ya kutua kutoka Ethiopia walipokubali kipigo cha bao moja lakini wakivuka kwa jumla ya mabao 2-1.
Nahodha huyo wa zamani wa mabingwa hao amewasifu wachezaji wake kwa moyo wa kujituma na kufuata maelekezo yao muda wote wa mchezo hadi kufikia hatua hiyo.
“Mechi ilikuwa ngumu sana, vijana walipambana kwa uwezo wao na walifuata maelekezo tuliyowapa mwisho wa siku tukafanikiwa.
“Hata bao la mapema lilituchanganya pia, tulipoteza mipira mingi kipindi cha kwanza lakini cha pili tulitulia tukacheza mpira wetu,” alisema Nsajigwa.
Nsajigwa na Noel Mwandila ndio waliisimamia timu kwenye mchezo huo kufuatia kocha mkuu George Lwandamina kutimkia nchini Zambia akihusishwa na kujiunga na Zesco United.