Katibu wa Halmashauri Kuu Itikadi na Uenezi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) Humphrey PolePole amesema kuna kiongozi mmoja wa upinzani amekuwa akizungumza uwongo na kuleta taharuki kwa wananchi kuhusu ripoti ya CAG na kusema inafaa achukuliwe hatua ili aache.
Kauli hiyo ameitoa jana Aprili 18, 2018 wakati akiongea na waandishi wa habari kuhusu kuwepo majadiliano kuhusu Ripoti ya CAG. Amesema wapo viongozi wa vyama vya siasa hawazungumzi juu ya mambo mazuri yaliyofanywa na serikali kama ujenzi wa miundombinu na mambo yanayopigwa hatua badala yake wamekuwa wakidakia mambo na kutoa taarifa za uongo.
“Sasa unaposoma taarifa za Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) halafu unatoa kauli timilifu kuwa pesa imeibiwa, yaani pesa ya Umma imeibiwa. Tunaweza tukakwambia tusaidie kuthibitisha sasa ukishindwa umesema uongo umeuhadaa Umma, umetoa takwimu za uongo ukichukuliwa hatua sio ndiyo utaanza kusema uongozi huu hatuna huruma, huruma kwa watu waovu? Waongo wanaopotosha kwa makusudi hilo halikubaliki”.Amesema Polepole
Akaendelea kusema, “Mimi sielewi huyu anayekwenda mbele kusema taarifa za uongo uongo hivi, ndiyo mtaji wake siku hizi anatafuta tu pahala. hoja hana, hazungumzi kuhusu rushwa siku hizi, hazungumzi kuhusu huduma za kijami, hazungumzi kuhusu ufisadi, hazungumzi kuhusu miundombinu, tunapiga hatua kubwa, tunapeleka watoto shule bure, bali yeye anatafuta hoja ya uongo uongo” amesema Polepole
“Kuna kipindi mtu huyu alizungumza kuhusu njaa, wewe unaijua njaa inatangazwa vipi sasa tumevumilia sana leo tumeshindwa tumeona tumsaidie kumuelewesha halafu tuseme wale ambao wana dhamana ya kuhakiki maneno tunayatoa kwa kweli wachukue hatua kwani hatupo tayari kuacha watu wachache waendelee kuudanganya umma wa watanzania hili halikubaliki” ameongeza