JESHI la Polisi nchini limeanza kufanya usaili kwa vijana walioomba kujiunga na jeshi hilo kutoka Jeshi la Kujenga Taifa (JKT) na Jeshi la Kujenga Uchumi (JKU).
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa jana na Msemaji wa Jeshi hilo, Barnabas Mwakalukwa, usaili huo utawahusu wale walioandika barua za maombi ya ajira ya kupitia kwa wakuu wao wa kambi za JKT na JKU na kupelekwa kwa makamanda wa Polisi wa mikoa.
Rais John Magufuli wakati akizindua ukuta wa Mirerani Aprili 6, mwaka huu, aliwaahidi vijana wa JKT waliojenga ukuta huo ambao hawakuwa na ajira kuwa watapata ajira.
"Kwa sababu sina cha kuwalipa, kuwalipa kwangu mimi ni nyie kupata ajira," alisema Rais Magufuli huku akiahidi kutoa barua ya kuwapongeza maofisa na askari waliofanya kazi ya ujenzi wa ukuta huo.
"Kwa hawa vijana wangu wa Operesheni Jakaya Kikwete na Operesheni John Magufuli, CDF (Mkuu wa Majeshi) alipokuwa anazungumza hapa nilikuwa nawaona wakuu wa vyombo wakitabasamu.
"Hii inadhihirisha kuwa ninyi mmejiuza wenyewe, nitahakikisha wale watakaofiti vizuri na ninavyowaona wote mmefiti vizuri basi tutakavyoweza kuwachukua muweze kuchukuliwa na kutumikia vyombo vyetu vya ulinzi na usalama," alisema Rais Magufuli.
Katika tarifa hiyo ya polisi, Mwakalukwa alisema wahusika walioomba moja kwa moja kwa Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini kupitia posta au makamanda wa polisi wa mikoa maombi yao hayatashughulikiwa na hawatafanyiwa usaili.
Akizungumza kwa njia ya simu na Nipashe jana, Mwakalukwa alithibitisha nafasi hizo kutolewa na jeshi hilo na kwamba vijana 1,500 wanataajiriwa kujiunga na Jeshi hilo.